Home – SDGs for All

A project of the Non-profit International Press Syndicate Group with IDN as the Flagship Agency in partnership with Soka Gakkai International in consultative status with ECOSOC

Watch out for our new project website https://sdgs-for-all.net

Wakenya Ni Wabunifu katika Kupata Njia za Kupambana na COVID-19

share
tweet
pin it
share
share

Na Justus Wanzala

BUSIA, Kenya (IDN) – Ni mchana wenye joto katika kituo cha mabasi katika kituo cha soko cha Mungatsi, Kaunti ndogo ya Nambale, katika Kaunti ya Busia, Magharibi mwa Kenya. Watu wengi, idadi kubwa yao wasafiri wanapanga foleni kuosha mikono yao. Kila mtu anadumisha umbali kutoka kwa mwingine wakati wanaosha mikono yao na kuabiri magari ya huduma za umma wakielekea maeneo yao mbalimbali.

Kuosha mikono kabla ya kuabiri magari ya huduma za umma na kudumisha umbali wa kijamii ni matendo mapya ambayo Wakenya wanalazimika kufuata. Imetajwa kuwa ya lazima na mamlaka ya afya kama hatua ya usalama kudhibiti kuenea kwa COVID-19.

Kwa hivyo, kuangalia haraka jinsi wanavyoosha mikono yao kunadhihirisha kitu kigeni. Abiria wanaosha mikono kwa kutumia vifaa vya usafi ambavyo vina vikanyagio ambavyo wakati vinasukumwa na mguu vinatoa maji kwenye ndoo iliyo kwenye kifaa cha chuma na sabuni ya kioevu moja kwa moja mikononi mwao.  Hii inawawezesha kuosha mikono yao bila kugusa sehemu yoyote ya kifaa.   

Kifaa ni uvumbuzi wa vijana wawili kutoka kaunti. Waliunda kifaa ili kuwezesha watu kuosha mikono yao salama. Wawili hao, Bernard Dindi na Christopher Butsunzu, hawana mafunzo ya kiufundi isipokuwa elimu ya shule ya upili. Wanasema kwamba walihamasishwa kubuni kifaa hicho baada ya kugundua changamoto za kudumisha usafi kufuatia kuzuka kwa COVID-19.

Kisha wakafanya utafiti mtandaoni kutengeneza kifaa cha kuosha mikono ambacho kingeweza kusaidia kupunguza uenezi wa virusi vya korona.

Walipokuwa wakifanyia kazi wazo lao, nchi ilikuwa ikishuhudia kuongezeka maradufu kwa maambukizi muda mfupi baada ya uthibitisho wa kisa cha kwanza mnamo Machi 13, 2020. Kwa kweli, viwango vya maambukizi vimeendelea kuongezeka kwa haraka na walioambukizwa kufikia 296 na waliopona 74 mnamo Aprili. 21, 2020

Wawili hao wanasimulia kwamba kifaa hupunguza hatari inayowakabili watu wanaotumia sabuni za kawaida. “Kwa kawaida, watu wanapoosha au kusafisha mikono yao, lazima waguse chupa na sabuni na mabomba ya maji. Tuliona hatari wanayokumbana nayo ya kuambukizwa na kueneza virusi,” walielezea.

Wakati wa kutumia kifaa hicho, mtu anasukuma tu kikanyagio cha kwanza kilicho chini ya mashine na kioevu cha kusafisha kinatoka na kisha anasukuma kikanyagio cha pili ili kutoa maji.

Dindi anasema waliamua kuweka kifaa cha kwanza kwenye kituo cha mabasi cha uwanja wa soko la mtaani kwa matumizi ya umma bure kwa sababu waligundua eneo hilo lina watu wengi walio katika hatari ya kuambukizwa. “Ni eneo lililo na watu wengi ndio maana tuliona kifaa kitasaidia,” anasema Dindi.

Anaongeza kuwa watu wengi wanaona ni cha kirafiki kwa mtumiaji.

“Nimekuwa nikikitumia kila siku tangu kusakinishwe. Ninaona ni rahisi kukitumia, “anasema Anne Nekesa, mfanyabiashara katika soko la Mungatsi. “Tunashangazwa na teknolojia ambayo vijana hawa wameendeleza. Hiki kinavutia sana, na tunafurahi kukihusu. Tunajisikia salama kuosha mikono yetu,” anasema John Wandera, mfanyakazi wa basi.

Vijana hao wanasema vifaa hivyo viliwagharimu angalau Shilingi elfu kumi za Kenya (dola 100) na siku kadhaa kutengeneza.

Kwa kutiwa moyo na mwitikio mzuri kutoka kwa watumiaji, wanalenga kutengeneza zaidi na kuvisambaza kote nchini.

“Tumeweza tu kutengeneza chache kwa sababu ya rasilimali chache. Lakini tukipata msaada wa kifedha, tutatengeneza zaidi,” wanasisitiza.

Umma na maafisa wa kaunti wamekaribisha kifaa hicho.

Afisa mkuu wa kaunti ya Busia wa afya na usafi wa mazingira, Isaac Omeri anasifu kifaa akisema kuwa kitasaidia sana katika vita dhidi ya COVID-19, “Hiki ni kifaa cha kipekee kinachopunguza nafasi ya mtu kuambukiza virusi wakati wa kuosha na kusafisha mikono yake,” anasema.

Tayari amenunua vifaa sita, ambavyo vitatumika katika ofisi mbalimbali za afya ndani ya kaunti.

Hakika, Kenya inavyoweka hatua za kudhibiti kuenea kwa COVID-19, uvumbuzi unaonekana kuwa njia inayopendelewa.

Mwanzoni mwa mwezi huu wa Aprili, Chuo Kikuu cha Kenyatta, kilicho karibu na mji mkuu wa Kenya, Nairobi, kilitangaza kwamba kimeendeleza kifaa cha kusaidia kupumua ambacho kinaweza kuokoa maisha ya waathiriwa wa virusi vya korona.

Vifaa vya kusaidia kupumua ni vifaa muhimu kwa wagonjwa wa virusi vya korona ambao hupata ugumu wa kupumua. Kwa bahati mbaya, ni vichache tu nchini Kenya.

Kama matokeo, wanafunzi wa chuo kikuu walikuja na mfano unaoitwa Tiba Vent (Tiba ni neno la Kiswahili kumaanisha treat (tiba).

Wanafunzi wapatao 16 kutoka vitivo tofauti waliendeleza mfano huo, kitengo cha mchemraba chenye sehemu za plastiki ngumu ya rangi ya fedha kilicho na mifereji inayounganisha na tanki la oksijeni na mifereji mingine miwili inayotoa hewa. Kinaunganishwa pia na monita ya kompyuta. Makamu wa Chansela wa Chuo Kikuu hicho, Paul Wainaina alisema chuo kikuu kinaweza kutoa vifaa 50 vya kusaidia kupumua kwa wiki.

Isitoshe, Taasisi ya Utafiti wa Matibabu ya Kenya (KEMRI) pia ilianza kutengeneza vifaa vya uchunguzi wa haraka wa COVID-19 mapema Aprili ili kuharakisha kupima COVID-19.  Taasisi ina kitengo cha uzalishaji chenye uwezo wa kutengeneza vifaa vya kupima vya kimatibabu na visafishaji vya mkono.

Makampuni kadhaa pia yanatengeneza barakoa za matumizi ya wafanyakazi wa umma na matibabu pamoja na Vifaa vya Kujikinga vya Kibinafsi (PPEs), ambavyo miezi michache iliyopita viliagizwa kutoka nje.

Mbali na hilo, serikali imeweka mkakati wa mbinu nyingi wa kudhibiti COVID-19 unaojumuisha hatua nyingi. Imeongeza ufuatiliaji katika vituo vyote vya kuingia, vituo vya afya na jamii kote nchini. Imesimamisha watu kusafiri kwenda nje na kuingia kaunti nne kati ya 47 nchini na kuanzisha upimaji wa halaiki uliolenga maeneo yenye idadi kubwa ya matukio ya COVID-19.

Wananchi pia wamehimizwa kuendelea kuwa macho kwa kuwa hatari bado iko juu na wameshauriwa kuendelea kuchukua hatua za tahadhari kwa kudumisha usafi wa mikono na kupumua, mazoea salama ya chakula, kudumisha kutotangamana kwa kijamii na kujiepusha kukaribia watu wanaougua sana maambukizi ya kupumua.

Kwa wakati huu, kuvaa barakoa katika maeneo ya umma kumetangazwa kuwa lazima wakati taasisi zote za masomo zimefungwa. Vile vile yaliyopigwa marufuku ni mikutano ya hadharani na ya kibinafsi inayohusisha halaiki ya watu.

Tayari, shilingi bilioni mbili za Kenya (USD 200m), zimetengwa kupigana na COVID-19. Vituo vya kushughulikia wagonjwa pia vimeanzishwa katika kaunti zote 47 za nchi ingawa wengi wanakabiliwa na changamoto ya vifaa muhimu. [IDN- InDepthNews – 27 Aprili 2020]

Picha: Abiria anaosha mikono kwa kutumia kifaa kipya kabla ya kuabiri gari la huduma ya umma katika Kituo cha Mabasi cha Uwanja wa Soko la Mungatsi, Kaunti ya Busia, Kenya. Hisani: Kevin Wafula.

NEWSLETTER

STRIVING

MAPTING

PARTNERS

Scroll to Top